- Mwanzo
- Kuhusu sisi
- Utawala
- Fursa za Uwekezaji
- Huduma Zetu
- Madiwani
- Miradi
- Machapisho
- Kituo cha Habari
MHE. MWEBEA AONGOZA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI MANISPAA YA SHINYANGA.
Na: Shinyanga MC
Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mhe. Zamda Mwebea, ameongoza maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika leo Juni 5, 2025 katika Soko la Nguzonane, Kata ya Kambarage, Manispaa ya Shinyanga, Maadhimisho hayo yaliambatana na zoezi la usafi wa mazingira katika maeneo ya soko hilo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho haya, Mhe. Mwebea ametoa wito kwa wananchi wa Manispaa ya Shinyanga kuendeleza utamaduni wa kufanya usafi wa mazingira yao ya nyumbani na maeneo ya kazi, ili kulinda afya za wananchi na kuhifadhi mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.
“Leo tunaadhimisha Siku ya Mazingira Duniani. Zoezi la usafi tulilofanya hapa ni sehemu ya kuwakumbusha wananchi kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira. Kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya mazingira safi na maisha bora ya mwanadamu. Wazazi wetu walitupandia miti na kutuachia mazingira rafiki; nasi tuendelee kupanda miti ili na vizazi vyetu vipate mazingira bora ya kuishi,” amesema Mhe. Zamda.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Maliasili na Mazingira wa Manispaa ya Shinyanga, Ndg. Ezra Manjerenga, amesema kaulimbiu ya mwaka huu inawahimiza wananchi kuepuka matumizi ya plastiki na kuhamasisha matumizi ya mifuko mbadala ili kulinda mazingira dhidi ya uharibifu unaotokana na taka zisizooza.
“Maadhimisho ya siku ya Mazingira kwa mwaka 2025 yanaongozwa na Kaulimbiu ya mwaka inasema: ‘Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo Tuwajibike Sasa; Dhibiti Matumizi ya Plastiki’. Ni wito wa kitaifa unaotufundisha kuchukua hatua sasa ili kulinda mustakabali wa mazingira yetu,” amesema Ndg. Manjerenga.
Maadhimisho haya ni sehemu ya jitihada za Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kuhamasisha ushiriki wa jamii katika kutunza mazingira na kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa vitendo.
Tanesco S, Mwanza Road
Anwani ya Posta: P.O.Box 28 Shinyanga
Simu: +255-28-2763213
Simu ya Mkononi: 0759 023 788
Baruapepe: md@shinyangamc.go.tz
Haki zote zimehifadhiwa@2018.Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga