- Mwanzo
- Kuhusu sisi
- Utawala
- Fursa za Uwekezaji
- Huduma Zetu
- Madiwani
- Miradi
- Machapisho
- Kituo cha Habari
Katika kuunga mkono juhudi za serikali juu ya kukabiliana na vitendo vya ukatili na kusaidia watoto wanaoishi mitaani, Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, kwa kushirikiana na shirika la Railway Children Africa, imezindua rasmi Dawati la Ustawi wa Jamii katika Stendi ya Mabasi ya Mkoa wa Shinyanga.
Akizungumza haya leo juni 20, 2025 katika hafla hiyo ya uzinduzi, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Bi. Neema Rwegoshola, amelipongeza shirika hilo kwa juhudi kubwa za kuwajali watoto waishio mitaani huku akisisitiza kuwa kila mwananchi ana wajibu wa kushirikiana na mradi huu ili kusaidia kupunguza ongezeko la watoto hao na kujenga taifa imara la baadaye.
“Tunapaswa kushikamana kama jamii na kuhakikisha watoto hawa wanapata msaada wanaouhitaji. Uwepo wa dawati hili utarahisisha utoaji wa huduma muhimu za ustawi wa jamii na kuwa daraja la matumaini kwa watoto walio katika mazingira magumu hususani eneo hili la standi,” amesema Bi. Rwegoshola.
Kwa upande wake, Meneja wa Mradi kutoka Shirika la Railway Children Africa, Bi. Irene Wampembe, amesema kuwa uanzishwaji wa ofisi hiyo ndani ya standi ni mkakati mahususi wa kufikisha huduma karibu zaidi na wananchi na kuwasaidia watoto wanaoishi mitaani huku akiongeza kuwa lengo ni kuelimisha jamii kuhusu madhara ya ukatili wa kijinsia, kuhamasisha malezi bora, na kufanikisha jitihada za kutokomeza vitendo vya kikatili na unyanyasaji.
Naye Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Ndg. Revocatus Rutunda, amesema halmashauri itaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha vitendo vya ukatili vinatokomezwa kabisa ndani ya manispaa ya shinyanga huku akilipongeza Shirika hilo kwa utekelezaji wa mradi huo ndani ya manispaa.
Uzinduzi wa Ofisi hii ndani ya manispaa ya shinyanga ni ushahidi wa dhamira ya dhati ya halmashauri katika kuhakikisha ustawi wa watoto na ustawi wa kijamii kwa ujumla unapata kipaumbele, hasa kwa wale wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Tanesco S, Mwanza Road
Anwani ya Posta: P.O.Box 28 Shinyanga
Simu: +255-28-2763213
Simu ya Mkononi: 0759 023 788
Baruapepe: md@shinyangamc.go.tz
Haki zote zimehifadhiwa@2018.Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga